Radiamali za kulalamikia kuendelea ukandamizaji unaofanywa na serikali ya Yemen

Sera za mabavu na ukandamizaji za watawala wa Yemen katika kukabiliana na malalamiko ya wananchi yanayodhihirishwa kwa njia za amani zimekabiliwa na radiamali za upinzani za harakati, vyama na shakhsia mbalimbali wa nchi hiyo. Msemaji wa harakati ya Ansarullah ametangaza kuwa Mahauthi hawatoruhusu serikali ya Yemen imwage tena damu za wapinzani wanaoandamana kwa amani. Kufuatia mashambulio ya kinyama yaliyofanywa na vikosi vya usalama vya Yemen dhidi ya wapinzani karibu na jengo la ofisi ya Waziri Mkuu, msemaji wa Ansarullah Muhammad Abdussalam, amesema serikali ya Yemen ndio msababishaji mkuu wa maafa hayo na kubainisha kuwa serikali hiyo haitaki kusikiliza sauti ya malalamiko yanayotolewa kwa njia za amani kwa sababu imeamua kusikiliza na kufuata amri kutoka nje ya nchi. Msemaji wa Ansarullah amesisitiza kwa mara nyengine juu ya ulazima wa kuendelezwa harakati ya malalamiko ya wananchi hadi kuhakikisha matakwa ya wananchi hao yanatekelezwa. Inafaa kuashiria hapa kuwa juzi Jumanne vikosi vya usalama na jeshi vikiandamana na watu waliobeba silaha walioziba nyuso zao waliyashambulia maandamano ya amani ya wananchi katika mji mkuu wa Yemen, Sana’a, wakawafyatulia risasi wananchi hao ambao hawakuwa na lengo jengine ghairi ya kufunga mahema yao mbele ya jengo la ofisi ya Waziri Mkuu na kukusanyika hapo hadi matakwa yao yatakapotekelezwa. Matokeo ya mashambulio hayo ya vikosi vya serikali yalikuwa ni kuuawa raia kumi na kujeruhiwa makumi ya wengine. Takwa kuu la wananchi wanamapinduzi wa Yemen ni kuondolewa serikali mbovu iliyopo na kuundwa serikali mpya yenye uwezo wa kuihudumia nchi kulingana na misingi ya makubaliano yaliyofikiwa katika mazungumzo ya kitaifa na kuutatua mgogoro na hali mbaya ya kiuchumi inayotawala nchini humo.
Kwa mujibu wa Hassan As Sa’adi, mjumbe wa baraza la kisiasa la harakati ya Ansarullah ya Yemen, baadhi ya madola ya kigeni ambayo yana hofu ya kuwepo demokrasia nchini Yemen yanaishinikiza serikali ya Sana’a iwakandamize vikali wapinzani ili serikali hiyo isiweze kulegeza kamba katika msimamo wake. As Sa’adi mbali na kusisitiza kwamba matokeo mabaya yanawangojea watawala wa Yemen amefichua pia kuwa watu wa karibu na makundi ya kitakfiri na al Qaeda wamekuwa wakihudumu kwenye vikosi vya usalama vya nchi hiyo. Ali Al Bukhaiti, mjumbe mwengine wa baraza la kisiasa la harakati ya Ansarullah, naye pia amesisitiza kwamba harakati ya Mahuthi itaendelea kufanya mikusanyiko zaidi ya upinzani katika mji mkuu na kandoni mwa majengo ya wizara hadi kuhakikisha serikali inang’atuka madarakani. Jumuiya ya Maulamaa wa Yemen nayo pia imetoa taarifa ya kulaani mashambulio ya siku ya Jumanne dhidi ya wafuasi wa harakati ya Ansarullah waliokuwa wamekusanyika kwa amani katika barabara ya al Matar na kueleza kwamba Wizara ya Mambo ya Ndani ndiyo inayobeba dhima ya damu iliyomwagwa ya raia wasio na hatia. Muhammad al Maqalih, mjumbe wa kamati kuu ya chama cha Kisoshalisti cha Yemen yeye amesema kuhusiana na matukio yaliyojiri mjini Sana’a na mashambulio ya vikosi vya usalama dhidi ya raia, kwamba kilichotokea katika mji mkuu huo wa nchi hiyo ni mauaji ya halaiki kwa maana yake halisi na kwamba rais ndiye anayebeba dhima hiyo.  Hayo yanajiri katika hali ambayo vitendo vya mabavu vya serikali ya Yemen dhidi ya harakati za amani za wapinzani vimelalamikiwa na duru za kidiplomasia pia ambapo msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameeleza wasiwasi alionao kutokana na utumiaji nguvu na mabavu wa vikosi vya usalama vya Yemen dhidi ya malalamiko ya wananchi. Bi Marzie Afkham aliyasema hayo jana na kuitaka serikali, vyama vya siasa na makundi mbalimbali ya Yemen wajidhibiti katika uchukuaji hatua; na akaongeza kwa kusema utatuzi wa masuala yaliyopo utapatikana kwa njia ya mazungumzo tu; na kwa kupitia mchakato wa kisiasa na wa njia za amani utakaoshirikisha vyama, makundi na harakati zote za kisiasa na kijamii za Yemen ndipo itawezekana kurejesha uthabiti, amani na utulivu nchini humo…/