Mahakama maalumu mjini Riyadh, Saudi Arabia, leo imeahirisha
hukumu dhidi ya Sheikh Nimr Baqir an Nimr ambaye anaendelea kushikiliwa katika
korokoro za utawala wa Aal Saud kwa miaka miwili sasa. Habari zinasema kuwa,
mahakama hiyo imeahirisha hukumu ya Sheikh Nimr Baqir an Nimr hadi mwishoni mwa
mwezi huu baada ya kufanya kikao na kujadili tuhuma zinazomkabili Sheikh Nimr.
Hii ni baada ya kutolewa onyo kutoka kwa viongozi wa kidini wakiwemo maraajii
wa Kiislamu katika nchi tofauti wakiuonya utawala wa nchi hiyo ya kifalme
kuhusu uwezekano wa kumuhukumu adhabu ya kifo mwanachuoni huyo. Mbali na
maulamaa wa Kiislamu, nchi kadhaa za Kiarabu na asasi za kutetea haki za
binaadamu nazo zilikuwa zimeonya kuwa huku kama hiyo itazusha hasira ndani ya
nchi hiyo. Duru za habari nchini Iraq zimetangaza kuwa Ayatullahil Udhma Sayyid
Ali Sistani amemtaka rais wa nchi hiyo Fuad Masum, kuchukua hatua za haraka za
kuzuia hukumu ya adhabu ya kifo inayoweza kutolewa na mahakama ya Saudia dhidi
ya shakhsia huyo wa kidini. Hii ni katika hali ambayo Ayatullah Naser Makarim
Shirazi, mmoja wa wanavyuoni wakubwa wa Kiislamu na marjaa wa kidini wa mjini
Qum hapa Iran alikuwa ametangaza kuwa, kutolewa adhabu ya kifo dhidi ya Sheikh
Nimr Baqir an Nimr, kutajeruhi
nyoyo za Waislamu wa Kishia kote ulimwenguni na kutakuwa na matokeo mabaya
sana. Marjaa huyo ameuusia utawala wa Aal Saud kusikiliza matakwa ya wananchi
wa nchi hiyo badala ya kutumia mabavu katika kuzima madai yao.