Khatibu
wa Sala ya Ijumaa iliyosaliwa mjini Tehran Hujjatul Islam Kadhim
Siddiqi amesema kuwa, mgogoro wa Ghaza ni kadhia nyeti zaidi katika
ulimwengu wa Kiislamu hivi sasa. Aidha amelaani vikali jinai za kinyama
za utawala haramu wa Kizayuni dhidi ya raia wa Palestina wasio na ulinzi
wa eneo hilo na kusisitiza kuwa, jinai za siku 30 sasa dhidi ya ukanda
huo ambazo ni jinai zisizo na kifani, zimeudhihirishia
ulimwengu kwamba utawala wa Kizayuni, hauheshimu hata kidogo sheria za
kimataifa. Vile vile khatibu wa sala ya Ijumaa ya mjini ya Tehran
amebainisha kwamba, Israel haisiti hata chembe kufanya jinai na kwamba
mauaji ya hivi sasa ya watu 2,000 na kuwafanya makumi ya maelfu ya
wengine kuwa wakimbizi, ni jinai ambazo hazina mfano wake katika
historia ya utawala huo. Hujjatul Islam Kadhim Siddiqi ameonyesha
kusikitishwa kwake na kimya cha taasisi za kimataifa ukiwemo Umoja wa
Mataifa kutokana na jinai za Israel huko Ghaza kwa kusema kuwa, taasisi
hizo kubwa duniani zilionekana kwamba ziliasisiwa kwa lengo la kuzitetea
nchi zinazodhulumiwa, hata hivyo kwa bahati mbaya kabisa, tunaziona
taasisi hizo hizo zikifumbia macho jinai za utawala katili wa Kizayuni
dhidi ya raia wa Ghaza bali hata zinaunga mkono unyama huo. Aidha
ameupongeza muqawama wa watu wa ukanda wa Ghaza mbele ya mashambulizi ya
kikatili ya Israel na kuongeza kuwa, muqawama huo ni wa kuigwa.
Amekosoa pia mataimshi ya hivi karibuni ya Ban Ki moon, Katibu Mkuu wa
Umoja wa Mataifa aliyetaka kuachiliwa huru askari mmoja wa Kizayuni
aliyetekwa nyara na wanamapambano wa Kipalestina wakati wa vita hivyo na
kusema kuwa, matamshi hayo yanatia huzuni sana. Amehoji kwamba,
inakuwaje mamia ya watoto wadogo wasio na hatia wanauliwa kinyama na
askari hao wa Israel, lakini katibu huyo hasemi chochote bali anathubutu
kutoa kauli ya kulaani kutekwa nyara askari mmoja tu wa utawala huo?