MASHAMBULIZI MAKUBWA YA ISRAEL KATIKA UKANDA WA GHAZA.





Katika hali ambayo fikra za walio wengi duniani katika wiki za hivi karibuni zimekuwa zikijielekeza zaidi kwa harakati za magaidi wa kitakfiri huko Iraq na Syria, utawala wa Kizayuni ambao ulikuwa ukisubiri kupata fursa ya kuendeleza jinai zake dhidi ya Wapalestina wasio na ulinzi wala hatia, hivi sasa umeziweka katika ajenda yake kuu chokochoko zake mpya huko Palestina. Masuala hayo yanadhihirisha wazi kwamba eneo la Mashariki ya Kati lingali linakabiliwa na hatari kubwa kutoka kwa Wazayuni na matakfiri. Vyombo vya habari vimeripoti kuwa, jeshi la utawala wa Kizayuni limeanzisha mashambulio makubwa ya anga katika eneo la Ukanda wa Ghaza. Baada ya Baraza la Mawaziri la utawala wa Kizayuni kuidhinisha kushadidishwa mashambulizi huko Ghaza, ndege za kivita za utawala huo juzi usiku ziliyashambulia karibu maeneo yote ya Ukanda wa Ghaza. Usiku wa kuamkia leo Jumatano pia, utawala katili wa Kizayuni umefanya mashambulizi ya kinyma huko Ghaza na kuwaua shahidi Wapalestina kadhaa. Baadhi ya vyombo vya habari vya Kiarabu vimeripoti kuwa, operesheni ya nchi kavu ya jeshi la utawala wa Kizayuni huko Ghaza ambayo imepewa jina la "mwamba mgumu" imeanza sambamba na mashambulizi ya anga ya jeshi la utawala huo. Baraza la Mawaziri la Israel lilitangaza katika kikao chake cha dharura kuwa, jeshi la utawala huo litazidisha mashambulizi dhidi ya raia wa Palestina. Hii ni katika hali ambayo utawala wa Kizayuni katika siku za hivi karibuni pia umezidisha vitisho vyake kwa raia wa Palestina na kuzusha tuhuma mbalimbali dhidi ya Wapalestina ili kuhalalisha hatua yake ya kushadidisha mashambulizi dhidi ya wananchi wa Palestina wa Ukanda wa Ghaza. Kivyovyote vile, jinai zinazofanywa na utawala wa Kizayuni kupitia mashambulizi ya pande zote huko Ghaza ni ukumbusho wa mashambulizi ya huko nyuma ya utawala huo dhidi ya Ghaza, mashambulizi yaliyopelekea utawala huo utende jinai za kutisha dhidi ya Wapalestina. Kuendelea uchokozi huo wa utawala wa Kizayuni huko Ghaza ni sawa kabisa na kukiuka makubaliano ya usitishaji vita yaliyofikiwa kati ya utawala wa Kizayuni na Wapalestina baada ya kushindwa utawala huo katika vita vya siku 8 ulivyovianzisha dhidi ya Ghaza mwishoni mwa mwezi Novemba mwaka 2012. Utawala wa Kizayuni unaendeleza mashambulizi yake dhidi ya Wapalestina katika hali ambayo kwa mujibu wa makubaliano ya huko nyuma, Israel inapaswa kujiepusha na uchokozi wa aina yoyote ile au kutoa vitisho vyovyote dhidi ya raia wa Palestina. Hii ni katika hali ambayo, kabla ya kufikiwa usitishaji vita wowote au makubaliano ya amani kati ya Wapalestina na utawala wa Kizayuni, walimwengu wanashuhudia kushtadi jinai za utawala huo ghasibu na suala hilo linadhihirisha wazi namna Israel isivyoheshimu masuala kama amani wala usitishaji mapigano. Upuuzaji na kimya cha jamii ya kimataifa kwa ombi la Wapalestina ambao daima mwamekuwa akitaka kudhaminiwa usalama wao kwa kufikiwa usitishaji vita wa kudumu na kuulazimisha utawala wa Kizayuni uheshimu makubaliano hayo, yote hayo yameitia kiburi Israel cha kuendeleza mshambulizi yake ya kikatili dhidi ya Wapalestina. Utawala wa Kizayuni unaendeleza jinai na mashambulizi yake katika Ukanda wa Ghaza kwa malengo maalumu moja likiwa ni kufelisha mchakato wa umoja wa kitaifa kati ya Wapalestina. Hata hivyo uzoefu wa vita vya huko nyuma vilivyoanzishwa na utawala wa Kizayuni katika eneo hili vikiwemo vita vya siku 22 vilivyoanzishwa na Wazayuni dhidi ya Wapalestina wa Ghaza vya mwaka 2009 na vile vya siku Nane dhidi ya eneo hilo mwaka 2012 unaonyesha kuwa, mashambulizi mapya ya hivi sasa ya utawala wa Kizayuni hayatakuwa na lolote ghairi ya kugonga mwamba tu kutokana na kushindwa mara kadhaa Israel mbele ya muqawama wa wananchi wa Palestina. Kuendelea jinai hizo na vitendo vya kujitanua vya utawala wa Kizayuni katika mwaka huu pia kunabainisha wazi kuwa, Wapalestina na hasa wakazi wa Ukanda wa Ghaza wangali wanakabiliwa na chokochoko na jinai za Israel. Mazingira kama hayo yanatoa udharura kwa jamii ya kimataifa kuchukua hatua kali na za haraka ili kuushinikiza utawala wa Kizayuni usitishe jinai zake hizo dhidi ya wananchi wa Palestina wasio na ulinzi wala hatia wa Ukanda wa Ghaza.