JUMUIYA YA WAISLAMU NCHINI NIGERIA YAALANI MAUAJI YA WAISLAMU WA KISHIA.

Jumuiya ya Waislamu nchini Nigeria imelaani mauaji ya Waislamu wa Kishia yaliyotekelezwa katika siku ya kimataifa ya Quds. Kwa mujibu wa ripoti hiyo jumuiya hiyo imelaani mauaji hayo iliyoyataja kuwa ya kinyama. Aidha jumuiya hiyo imeongeza kuwa, hakuna sababu yoyote ya kuhalalisha mauaji hayo hasa kwa kuzingatia kuwa, Waislamu hao wa Kishia waliuawa wakiwa wanaandamana kwa amani katika siku hiyo ya kimataifa ya Quds. Jumuiya hiyo ya Waislamu wa Nigeria imesisitiza kuwa, ni jukumu la serikali kutoa mwanya kwa wafuasi wa dini kutekeleza matukufu yao bila kizuizi chochote. Hii ni katika hali ambayo Harakati ya Waislamu wa Kishia nchini Nigeria, imeituhumu serikali ya Abuja kwa kuandaa mpango wa kutekelezwa mauaji hayo ya mjini Zaria katika jimbo la Kaduna. Tukio hilo lilitokea wakati Waislamu wa Kishia walipoungana na Waislamu wengine duniani katika maandamano ya kimataifa ya siku ya Quds mjini hapo ambapo polisi walianza kuwamiminia risasi waandamanaji na kuua watu 33 akiwamo mtoto mmoja wa Sheikh Ibrahim Zakzaky, kiongozi wa jamii ya Waislamu wa Kishia nchini humo. Aidha katika tukio hilo idadi ya Waislamu wengine walijeruhiwa huku watoto wawili wa sheikh huyo wakitekwa nyara na kupelekwa kusikojulikana, ambapo nao waliuawa muda mchache baadaye. Kwa mujibu wa uchunguzi uliofanywa na Waislamu hao, askari wa serikali walitoka mjini Abuja wakiandamana na magari ya kijeshi mjini Zaria kwa lengo la kutekeleza hujuma hiyo.