WATU WANAFIKIRI HAWATAPATA MISUKOSUKO KWA VILE WAMEAMINI:

Wakati Mwenyezi Mungu alipoteremsha maneno yake yasemayo: “Alif lam Miym. Je, watu wanadhani wataachwa (wasitiwe katika misukosuko) kwa kuwa wanasema: “Tumeamini” Basi ndio wasijaribiwe?” (Qur’an 29:1-2). Imam Ali bin Abi Talib (a.s) anasema: Nilitambua ya kwamba fitina haitotushukia wakati Mtume (s.a.w.w) akiwa pamoja nasi. Nikasema: “Ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu, je wewe hukuniambia siku ya vita vya Uhud wakati walipouawa Mshahidi miongoni mwa Waislamu, na mimi nikanyimwa kuuawa Kishahidi, na nikaudhika kwa hilo (kutokuuawa Kishahidi).” Ukaniambia: “Furahia, kwani kuuwa Kishahidi kuko nyuma yako.” Aliniambia: “kwa hakika jambo hilo litatokea tu, basi itakuwaje uvumilivu wako wakati huo? Nikasema: “Ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu! Jambo hili (kuuawa Kishahidi) si katika mambo yanayohitaji uvumilivu (subira), bali ni katika mambo ya furaha na kushukuru.” Akasema: “Ewe Ali! Kwa hakika watu watafitinishwa kwa mali zao baada yangu, na watamsimanga Mwenyezi Mungu kutokana na imani zao na huku wakitarajia Rehema zake na kujiaminisha dhidi ya adhabu yake, na watajihalalishia aliyoyaharamisha ulevi kwa kuuita maji ya shayiri, na kitolewacho kwa njia ya haramu kukiita zawadi, na riba kuitwa ni biashara.” Nikasema: Ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu! Ifikapo hali hiyo, niamiliane nao vipi! Niamiliane nao kama waliotoka katika Uislamu au niamiliane nao kama waasi? Alisema: “Amiliana nao kama waasi.”