'TAIFA LA IRAN HALITAYAPIGIA MAGOTI MADOLA MAKUBWA'



Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa, iwapo taifa la Iran litajikita katika kuimarisha uwezo wa ndani ya nchi, basi Marekani na madola mengine makubwa hayawezi kuthubutu kufanya chochote dhidi ya nchi hii. Ayatullahil Udhma Sayyid Ali Khamenei ameyasema hayo leo Jumanne mjini Tehran alipokutana na maelfu ya watu kutoka mkoa wa Ilam. Sambamba na kutoa salamu za kheri na fanaka kwa mnasaba wa kukumbuka kuzaliwa Imam Ali AS, Kiongozi Muadhamu ameongeza kuwa, kwa kutumiwa uwezo wa ndani ya nchi, Marekani na madola mengine makubwa duniani kamwe hayataweza kulishinikiza taifa la Iran kwa njia za kijeshi au zisizo za kijeshi. Ameongeza kuwa, madola makubwa yafahamu kuwa taifa la Iran halitayapigia magoti kwani taifa hili liko hai na vijana wake wako katika harakati ya mkondo sahihi.  Kiongozi Muadhamu amesema utekelezwaji sera za 'uchumi wa kimapambano' na kutegemea uwezo wa ndani ya nchi ndio njia sahihi ya kutatua matatizo ya kiuchumi. Ayatullah Khamenei amesema pale ubunifu na umahiri wa vijana unapotegemewa, ustawi hupatikana. Ametoa mfano wa mafanikio ya kivitendo yaliyopatikana Iran kwa kutegemea vijana na kutaja ustawi katika sekta za nyuklia, dawa, seli shina, teknolojia ya nano na utengenezaji zana za kujihami. Ameendelea kusema kuwa vijana wa Iran wanavutiwa na Uislamu, Qur'ani, umaanawi na mapenzi kwa nchi. Ayatullahil Udhma Khamenei amesema moja ya somo tunalopata kutoka kwa Imam Ali AS ni kujitahidi katika kuleta saada ya kweli katika jamii kwa kutatua matatizo ya kimaisha na kiuchumi ya wananchi. Amesema hilo linawezekana kwa kuwepo mipango sahihi na kutumia uwezo mkubwa wa vijana nchini Iran. Chanzo cha habari (irib)