RAIS WA IRAN ANAPASWA AWE MTIIFU KWA ALLAH (S.W.T).


Khatibu wa muda wa Sala ya Ijumaa ya hapa mjini Tehran amesema kuwa, kukubali misingi ya dini, kutii msingi wa "Wilaya," maadili mema na kuheshimu sheria, ni mambo muhimu anayotakiwa awe nayo rais ajaye wa Iran. Ayatullah Khatami amesema kuwa, ikiwa rais atakayechaguliwa nchini, atakuwa mwenye kukubaliana na misingi ya dini, utawala wa faqihi na kufuata sheria, kamwe hatokubali nchi hii ikanyagwe na maadui na pia hatolegeza misimamo mbele ya vitisho vya maadui. Ameitaja kazi ya kumchagua rais wa baadaye wa Iran kuwa inahitaji kufanywa kwa umakini na uangalifu mkubwa na kuongeza kuwa, ikiwa taifa la Iran litawachunguza vizuri wagombea watakaoshiriki katika uchaguzi wa mwaka huu, bila ya shaka yoyote litaweza kumpata mtu mwema zaidi na anayefaa zaidi kuliongoza taifa hili. Aidha Khatibu wa Sala ya Ijumaa iliyosaliwa leo hapa mjini Tehran ameashiria njama za wakoloni na utawala haramu wa Kizayuni, za kujaribu kuzuia ushiriki mkubwa wa wananchi katika uchaguzi wa rais wa mwezi Juni mwaka huu hapa nchini na kusisitiza kuwa, mabeberu wa dunia wanakusudia kuharibu anga huru ya kufanyika uchaguzi nchini Iran na hivyo kuchafua sura ya taifa hili kimataifa. Lakini amesisitiza kuwa, njama hizo zitavunjwa na hamasa kubwa ya wananchi katika uchaguzi wa tarehe 14 Juni mwaka huu. Kuhusiana na matukio yanayoendelea huko Syria na jinai ya kuvunjia heshima haram ya sahaba wa Mtume Muhammad (SAW) Hujri bin Adi (RA), Ayatullah Ahmad Khatami amesema kuwa, hatua ya maulama wa Kisuni na Kishia duniani ya kulaani kitendo hicho kiovu inaonyesha kuwa maulama hao wako macho dhidi ya fitina za kimadhehebu na vitendo vyovyote vya kuzusha mizozo na mifarakano katika safu za Waislamu. Kuhusiana na mashambulizi ya hivi karibuni ya ndege za utawala wa Kizayuni wa Israel nchini Syria amesema kuwa, mashambulizi hayo yamefichua jinsi wapinzani wanaopigana dhidi ya serikali ya Damascus walivyo wasaliti kutokana na kushirikiana kwao na utawala wa Kizayuni dhidi ya taifa na watu wa Syria. Habari kutoka http://kiswahili.irib.ir/habari/iran/item/31757-rais-wa-iran-anapaswa-awe-na-maadili-mema-na-mtiifu-kwa-allah