'NJAMA ZA WAMAGHARIBI DHIDI YA IRAN ZIMEFELI'

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, Ayatullahil-Udhmaa Sayyid Ali Khamenei, amesema kuwa njama za Marekani na nchi za kikoloni za kujaribu kuipigisha magoti Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kuhusiana na kadhia ya nyuklia zimefeli. Kiongozi Muadhamu ameyasema hayo alipokutana na maulama, wanazuoni, wanafikra na wageni walioshiriki katika kongamano la kimataifa kuhusu ‘Tishio la Makundi ya Kitakfiri na yenye Misimamo ya Kufurutu Mipaka kwa Mtazamo wa Maulama wa Kiislamu’ kongamano lililofanyika mjini Qom nchini hapa ambapo sambamba na kuashiria mazungumzo ya nyuklia kati ya Iran na kundi la 5+1 amesema kuwa, licha ya Marekani na wakoloni wa Ulaya kuungana katika njama za kulishinikiza taifa hili liwapigie magoti kuhusu kadhia ya nyuklia, lakini wameshindwa na hawatofanikiwa. Akizungumzia ongezeko la makundi ya kufurutu mipaka katika miaka ya hivi karibuni yaliyoundwa na madola ya kibeberu kwa ajili ya kupambana na Uislamu, Kiongozi Muadhamu amesema kuwa vitendo vya makundi hayo machafu ya kitakfiri, vinafanyika kupitia mipango maalumu ya madola hayo ukiwemo utawala haramu wa Kizayuni, lengo kuu likiwa ni kuwasahaulisha Waislamu na walimwengu kwa ujumla kadhia ya Palestina na msikiti wa al-Aqsa. Amefafanua kuwa, kuanzishwa mwamko wa kielimu, kimantiki na kueneza elimu na umoja kwa ajili ya kung’oa mizizi ya harakati hizo za kitakfiri, kuweka wazi njama za kisiasa za madola ya kibeberu katika kuanzisha makundi hayo ya kitakfiri na kigaidi na kuzidisha uzingatiaji wa umma wa Kiislamu katika masuala yao muhimu hasa kadhia ya Palestina, ni miongoni mwa wadhifa muhimu wa maulama katika ulimwengu wa Kiislamu, hii leo. Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, Ayatullahil-Udhmaa Sayyid Ali Khamenei amesema kuwa, kupotosha mwamko wa Kiislamu, kuharibu miundombinu muhimu katika nchi za Kiislamu na kuchafua sura ya Uislamu kupitia makundi ya kigaidi na kitakfiri, ni miongoni mwa malengo ya Marekani na waitifaki wake katika eneo la Mashariki ya Kati na kwamba, hatua ya madola hayo ya kutumia makundi ya kitakfiri nchini Iraq na Syria ni kutaka kupotosha mapambano dhidi ya utawala ghasimu wa Israel unaozikalia kwa mabavu ardhi za Palestina. Akiashiria hatua za mara kwa mara za ndege za Marekani kuwarushia silaha za kivita wapiganaji wa kundi la kitakfiri la Daesh waliozingirwa kila upande amesisitiza kuwa, Marekani inadai kuunda muungano wa kimataifa kwa ajili ya kupambana na kundi hilo la Daesh, katika hali ambayo ni huo uongo mtupu kwani lengo la muungano huo ni kuhakikisha kuwa mapigano kati ya Waislamu wenyewe kwa wenyewe havimaliziki. Hata hviyo amesema, maadui hao watashindwa tu katika njama zao hizo. Chanzo cha habari: http://kiswahili.irib.ir/habari/kiongozi/item/44727-njama-za-wamagharibi-dhidi-ya-iran-zimefeli