'MAPAMBANO NDIYO NJIA YA KUKABILIANA NA MABEBERU'


Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa, njia pekee ya kuweza kusimama imara kukabiliana na kambi ya kibeberu iliyo dhidi ya ubinadamu ni kuendeleza fikra ya "kupambana" na kambi hiyo.

Ayatullahil Udhma Sayyid Ali Khamenei amesema hayo leo wakati alipoona na Spika na Wabunge wa Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu (Bunge la Iran) na huku akiashiria namna mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu ulivyoundwa na jinsi ulivyoweza kudumu na fikra yake ya mapambano amesisitiza kuwa, haiwezekani kufikia kwenye malengo makuu na matukufu ya mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu pasi na kuendelea na fikra ya kupambana na kambi ya kibeberu.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu vile vile ametoa mkono wa pole kwa mnasaba wa kukumbuka siku aliyouawa shahidi Imam Musa al Kadhim AS na kuongeza kuwa, sababu inayoifanya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ishikilie msimamo wake wa kuendelea na mapambano si kwa kuwa inapenda vita, bali ni kwa sababu akili inahukumu kuwa, mtu ana wajibu wa kujiandaa vizuri wakati anapopita katika eneo lililojaa maharamia, na lazima awe na nguvu na uwezo wa kutosha wa kujilinda mbele ya maharamia hao.
Ayatullahil Udhma Khamenei ameongeza kuwa, ulimwengu wa leo umejaa maharamia wanaopora heshima, utambulisho na maadili ya kibinadamu na kubainisha kuwa: Mabeberu wamejiimarisha kielimu, kiutajiri na nguvu za kijeshi na kipropaganda na wanatumia vitu hivyo kuficha jinai zao kubwa kwa kujifanya wema mbele ya walimwengu, kumbe ni wasaliti wa ubinadamu na wanaendesha vita vya kikatili katika maeneo mbalimbali duniani.

Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imesema iko tayari kutumia uwezo wake wa kupambana na ugaidi katika kuisaidia Nigeria kuwanusuru wasichana zaidi ya 200 waliotekwa nyara na kundi la kitakfiri la Boko Haram. Katika mahojiano maalumu na Press TV, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran anayeshughulikia masuala ya Kiafrika na Kiarabu Hussein Amir-Abdollahian amesema Iran imefanya mazungumzo na maafisa wa Nigeria katika siku za hivi karibuni kuhusu kadhia hiyo. Amongeza kuwa Iran imelaani vikali utekaji nyara wa washichana wa shule nchini Nigeria. Afisa huyo wa Iran ameelezea matumaini yake kuwa vitendo vya kigaidi vitafika ukingoni kote barani Afrika. Wakati huo huo habari za hivi punde kutoka Nigeria zinasema magaidi wa Boko Haram wametekeleza hujuma iliyopelekea watu wawili kupoteza maisha katika mji wa Jos kati mwa nchi hiyo. Aidha imearifiwa kuwa siku ya Alkhamisi magaidi hao waliwaua watu 28 katika vijiji vilivyo katika jimbo la Borno kaskazini mwa Nigeria. Jimbo hilo ni kituo cha uasi wa Boko Haram. Wanamgambo wa Boko Haram wanawashikilia wasichana wa shule wapatao 223 waliotekwa nyara hivi karibuni katika Jimbo la Borno kaskazini mwa Nigeria. Boko Haram ni kundi lenye misimamo ya kufurutu mipaka nchini Nigeria ambalo kutokana na kuwa na ufahamu mbaya na potofu kuhusiana na Uislamu, limeitumbukiza nchi hiyo katika dimbwi la machafuko na mauaji sambamba na kuzusha hitilafu za kidini na kikabila nchini humo.  


Utawala wa Kizayuni wa Israel katika siku za hivi karibuni umebatilisha mamia ya vibali vya kuishi raia wa Palestina katika mji mtakatifu wa Quds unaokaliwa kwa mabavu na utawala huo. Kuhusiana na hatua hiyo ya kijuba ya Wazayuni, taasisi ya kutetea haki za Wapalestina inayojulikana kama 'Mithaq' imetoa ripoti inayoonyesha kuwa, Wizara ya Mambo ya Ndani ya utawala haramu wa Israel kati ya mwaka 2012 na 2013, ilibatilisha vibali 241 vya ukaazi kwa Wapalestina kwa madai kwamba mji huo ni makao ya Wazayuni. Taasisi ya Mithaq inasema hujuma hiyo dhidi ya Wapalestina inaendelea na kwamba Walowezi wa Kizayuni wanapewa nafasi za Wapalestina wanaofukuzwa Quds Tukufu. Taarifa ya taasisi hiyo inasema hatua hiyo ya Tel Aviv haina lengo lingine ghairi ya kuuyahudisha mji wa Quds unaobeba msikiti wa al-Aqsa ambao ni kibla cha kwanza cha Waislamu.
Ripoti ya taasisi ya kutetea haki za Wapalestina inaelezea unyama wanaotendewa raia wa Palestina wanaoishi katika mji wa Quds ikisema kuwa, waliofutiwa vibali vya kuishi mjini hapo wanakatiwa huduma zote muhimu yakiwemo maji, umeme na hata kuzuiwa matibabu katika vituo vya afya vya mji huo. Hali hiyo inawafanya kukosa la kufanya na hivyo kulazimika kuondoka kwa madhila makubwa. Mkuu wa taasisi ya Mithaq, Bw. Fiyras Swabah amesema kuwa, hatua ya utawala wa Kizayuni ya kuwapokonya vibali vya kuishi na kuwafukuza Wapalestina kutoka mji wa Quds ni kinyume cha sheria na mikataba yote ya kimataifa kama vile kipengee cha 43 cha Azimio la Hague (The Hague Convention) pamoja na kipengee cha nne cha Azimio la Geneva (Geneva Convention).
Uzandiki na uafriti wa Israel dhidi ya Wapalestina unafanyika katika hali ambayo utawala huo ghasibu umezidisha kasi ya ujenzi wa vitongoji vya walowezi katika ardhi za Wapalestina unazozikalia kwa mabavu. Ujenzi wa vitongoji ni miongoni mwa sababu zilizopelekea Rais wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina, Mahmoud Abbas, kuondoka kwenye meza ya mazungumzo na Wazayuni mwanzoni mwa mwezi uliopita. Abbas alisema mazungumzo yataendelea tu iwapo Israel itawaachia huru wafungwa wa Palestina pamoja na kusimamisha ujenzi wa vitongoji vya walowezi wa Kizayuni katika ardhi za Wapalestina ilizopora na kuzighusubu.
Hujuma na jinai za Wazayuni dhidi ya Wapalestina zinafanyika kwa baraka, ridhaa na himaya ya moja kwa moja ya Marekani na waitifaki wake ambao hujidai kuwa vinara wa kutetea haki za binadamu. Hii inadhihirishwa na kitendo cha wabunge wawili wa Marekani; Neil Johnson na David McNally cha kuungana na Wazayuni katika kuuvunjia heshima msikiti mtakatifu wa al-Aqsa hivi majuzi. Kitendo hicho kumewakasirisha viongozi mbalimbali wa Kiislamu kuanzia wale wa kidini hadi wale wa kisiasa. Nabih Berri, Spika wa bunge la Lebanon kwenye radiamali yake amewataka viongozi wote wa Kiislamu duniani kuongeza mashinikizo kwa utawala wa Kizayuni ili ukome kuuhujumu na kuuvunjia heshima msikiti wa al-Aqsa pamoja na matukufu mengine ya Kiislamu na yale ya Kikristo.