MAZUNGUMZO YA NYUKLIA, HAKI ZA BINADAMU KATIKA HOTUBA YA KIONGOZI MUADHAMU:

 
 Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Ayatullah Ali Khamenei jana 
alihutubia mjumuiko mkubwa wa maulamaa, wanazuoni na watu wa matabaka 
mbalimbali wa mkoa wa Qum sambamba na hauli ya 36 ya harakati ya 
kihistoria ya watu wa mji huo dhidi ya utawala wa Shah. Katika hotuba 
yake Kiongozi Muadhamu alisema kuwa moja ya mambo muhimu ya harakati 
hiyo ya watu wa Qum ni kutegemea imani yao kubwa kwa Mwenyezi Mungu 
sambamba na kuwa na maarifa na uoni wa mbali katika mazingira magumu ya 
kupambana na adui.
 
 Uzoefu wa kihistoria wa taifa la Iran kabla 
na baada ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu umeonesha kuwa, taifa hilo 
daima limekuwa likiwashinda maadui kwa kutegemea imani yake kubwa kwa 
Mwenyezi Mungu na kuwa na maarifa na kuona mbali. Ushindi wa Iran katika
 vita vya miaka minane vilivyoanzishwa na utawala wa Saddam, kuvuka 
vipindi na misukusuko mingi na migumu ya vikwazo na kuwa macho mbele ya 
njama mbalimbali za kisiasa katika kipindi cha miaka kadhaa iliyopita na
 kuweza kuzima njama hizo ni vielelezo vya wazi vya imani kubwa ya taifa
 la Iran na kuwa kwake makini katika vipindi mbalimbali vya uhai wa 
Mapinduzi ya Kiislamu hapa nchini.
 
 Miongoni mwa mambo 
yaliyoashiriwa na Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu katika 
hotuba yake ya jana ni mazungumzo ya nyuklia yanayoendelea kati ya Iran 
na kundi la 5+1. Amesisitiza kuwa mazungumzo hayo hayatokani na 
mashinikizo ya vikwazo bali Iran inafanya mazungumzo kwa mujibu wa 
maslahi yake.
 
 Baada ya kuja madarakani serikali mpya hapa 
nchini, suala la kuamiliana na mfumo wa kimataifa kwa mujibu wa 
kuheshimiana lilipewa kipaumbele katika siasa za nje za Jamhuri ya 
Kiislamu. Muamala mzuri wa Iran mkabala wa nchi za Magharibi ambao 
ulikaribishwa sana na watu wa Ulaya ulizilazimisha serikali za nchi za 
Magharibi kuketi kwenye meza ya mazungumzo ya nyuklia na Iran. Duru 
kadhaa za mazungumzo hayo ya Iran na kundi la 5+1 huko Geneva zimeonesha
 kwamba, Tehran haikuingia katika mazungumzo kwa sababu ya mashinikizo 
ya vikwazo.
 
 Kabla ya kuanza mazungumzo hayo nchi za Magharibi 
hususan Marekani zilitishia kuwa zingeshambulia taasisi za kuzalisha 
nishati ya nyuklia hapa nchini. Hata hivyo matokeo ya mazungumzo ya 
tarehe 24 Novemba 2013 yameonesha kuwa Wamagharibi hawana njia nyingine 
ghairi ya kuamiliana na Iran.
 
 Suala la haki za binadamu ni 
miongoni mwa mambo yaliyoashiriwa na Kiongozi Muadhamu katika hotuba ya 
jana. Amesema Wamarekani hawana haki ya kuzungumzia maudhui ya haki za 
binadamu kwa sababu serikali ya Marekani ndiyo mvunjaji mkubwa wa haki 
hizo duniani.
 
 Wamagharibi hususan Marekani wamekuwa wakitumia 
suala la haki za binadamu kwa ajili ya kufikia malengo yao nchini Iran. 
Hata hivyo ushahidi na nyaraka za kuaminika zinaonesha kuwa, wanaodai 
kuwa vinara wa haki za binadamu duniani ndio hao hao wavunjaji wakubwa 
wa haki hizo. Mauaji ya watoto wadogo na wanawake wa Afghanistan, 
Pakistan na Yemen kutokana na mashambulio yanayofanywa na ndege zisizo 
na rubani za Marekani (drone), mateso yaliyofanywa na Wamarekani dhidi 
ya wafungwa katika jela za Abu Ghuraib huko Iraq, Guantanamo Bay Cuba na
 Bagram huko Afghanistan na uungaji mkono wa Washington kwa jinai 
zinazoendelea kufanywa na utawala wa Kizayuni wa Israel dhidi ya taifa 
la Palestina ni sehemu ndogo tu ya ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu 
wa Marekani na waitifaki wake.
 
 Na Amir Ibrahim Rutajengwa. (irib)