Bismillah Rahmanir Rahiim



Mwenyezi Mungu (s.w.t) anasema: “Kwa sababu ya rehema itokayo kwa Mwenyezi Mungu, umekuwa laini kwao. Lau ungekuwa mkali mwenye moyo mgumu, bila shaka wangelikukimbia. Basi wasamehe na uwaombee maghfira na ushauriane nao katika mambo. Utakapoazimia, basi mtegemee Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu anawapenda wamtegemeao.” (Surat al-Imraan: 159)
Ikiwa unyenyekevu unatakiwa kwa kila mmoja wetu, basi Wanachuoni wa kidini wanafaa zaidi na wanastahiki zaidi kuwa na tabia hii njema, kutokana na kusoma kwao mafunzo ya Uislamu, na kujishughulisha kwao na ulinganiaji na uongozaji, na kwa nafasi ya kidini waliyonayo katika macho ya watu, ambapo mtazamo wa watu wengi kuhusu dini hupata kupitia mwonekano wao na mwenendo wao. Na kwa unyenyekevu na tabia yao njema wanaipa dini sura nzuri na mwonekano mzuri unaovutia nafsi za watu kwenye dini. Wanachuoni wakiwa wamepatwa na maradhi ya majivuno na kujikweza, watafeli katika jaribio la kuvutia nyoyo za watu, na watatoa mfano mbaya wa hali ya dini katika jamii.