MASHIA NA MASUNNI IRAQ WASWALI IJUMAA PAMOJA.

Maelfu ya Waislamu wa madhehebu ya Shia na Sunni nchini Iraq leo wamesimamisha sala ya Ijumaa pamoja kama njia ya kuimarisha umoja wa Kiislamu na kupinga mapigano ya kimadhehebu nchini humo.

Waislamu wa Iraq wameungana katika Sala ya Ijumaa katika maeneo mbali mbali nchini humo kufuatia wito wa Waziri Mkuu wa Iraq Nouri al Maliki ambaye amewataka Wairaqi Mashia na Masunni kuswali pamoja kama njia ya kusisitiza udharura wa umoja na mshikamano nchini humo.

Televisheni za Iraq zimeonyesha wanazuoni, wanasiasa na wananchi kutoka madhehebu ya Shia na Sunni wakiwa wamesimama pamoja katika safu za sala ya Ijumaa ili kuvunja njama za maadui ambao wamekuwa wakiibua hitilafu baina ya Waislamu nchini humo. Katika siku za hivi karibuni Iraq imeshuhudia hujuma za kigaidi ambapo mamia ya watu wamepoteza maisha. Magaidi hao wamekuwa wakiwalenga maafisa wa usalama na misikiti.